Pages

Monday, April 11, 2011

Aliyoyasema Hayati Edward Moringe Sokoine

Ndugu Edward Moringe Sokoine (01/08/1938-12/04/1984) alikuwa Waziri Mkuu wa aina yake nchini Tanzania. Aliongoza katika kipindi ambacho nchi ilikuwa katika hali ngumu sana ya kiuchumi. Leo ni miaka 27 toka Taifa limpoteze shujaa huyu. Katika kuenzi fikra zake ambazo bado zinahitajika sana leo, Udadisi inakuletea nukuu zifuatazo kama ilivyozipata kutoka kwenye Kitabu cha Edward Moringe Sokoine: Kiongozi wa Watu Aliyejitolea kilichoandikwa na Luteni Kanali Albert N. Kigadye mnamo mwaka 1984:






"Ole wake kiongozi mzembe na asiye na nidhamu nitakayemkuta: Kiongozi wa siasa hana usalama wa aina yoyote. Usalama wake ni kudra ya Mungu na Wananchi peke yake. Viongozi wazembe na wabadhirifu wahesabu siku zao. Labda tusiwajue. Hawa hatuna sababu ya kuwapa imani, kuwa tutawalinda kama vitendo vyao viovu" - Edward Moringe Sokoine, 26 Machi 1983





"Juu ya suala hili la mapato kutolingana na matumizi ni kwamba tungependa kupunguza uongezaji wa wataalam wasiohitajika katika Serikali na katika mashirika ya umma mpaka hapo hali yetu ya uchumi itakapokuwa katika hali nzuri" - Edward Moringe Sokoine, 23 Oktoba 1982





"Serikali inasimamia bei, lakini Serikali yetu itakwenda mpaka itasimamia bei ya mhogo, dagaa na bei ya kila kitu? Haiwezekani, vitu vingine ni lazima vizalishwe kwa wingi ili bei yenyewe iweze kujirekebisha" - Edward Moringe Sokoine, 24 Septemba 1983





"Wajibu wa kila Mtanzania, kila familia na kila anayekula ni kujilisha mwenyewe. Si wajibu wa Taifa kumlisha mtu. Unaweza ukasaidiwa unapopatikana na janga. Lakini kama hakuna janga ni wajibu wa kila mtu aweze kujitosheleza kwa chakula na atoe ziada kwa Taifa" - Edward Moringe Sokoine, 4 Oktoba 1983




Katika kuendeleza kumbukumbu ya sokoine hii nimeiona kwa kaka chambi nikaona na  nyie niwatundikie
pata aliyowahi kuyasema.
"Vijana leo wengi wana mali zaidi kuliko wazee waliofanya kazi miaka thelathini hadi arobaini. Lakini wanaitaka Serikali ndiyo iwaulize mali hiyo wameipata wapi. Hivi kwa nini mzazi asumuulize mwanae, 'mali hii umeipata wapi?'" - Edward Moringe Sokoine, 23 Oktoba 1983





"Katika nchi inayojali haki na usawa, majeshi hayana budi yawe ni chombo cha kulinda haki na maslahi ya walio wengi. Na kamwe hayaruhusiwi kuwa ni chombo cha wachache wenye kujali nafsi zao na kusahau maslahi ya walio wengi" - Edward Moringe Sokoine, 1Februari 1977

No comments: